Micah 7

Taabu Ya Israeli


1 aTaabu gani hii niliyo nayo!
Nimefanana na yule akusanyaye
matunda ya kiangazi,
aokotaye masazo baada ya kuvunwa
shamba la mizabibu;
hakuna kishada chenye matunda ya kula,
hakuna hata ile tini ya mwanzoni ninayoitamani.

2 bWanaomcha Mungu wameondolewa kutoka nchi;
hakuna mtu mnyofu hata mmoja aliyebaki.
Watu wote wanavizia kumwaga damu,
kila mmoja anamwinda ndugu yake kwa wavu.

3 cMikono yote miwili ni hodari katika kufanya ubaya,
mtawala anadai zawadi,
hakimu anapokea rushwa,
wenye nguvu wanaamuru wanachotaka:
wote wanafanya shauri baya pamoja.

4 dAliye mwema kupita wote kati yao
ni kama mchongoma,
anayeonekana mnyofu zaidi miongoni mwao
ni mbaya kuliko uzio wa miiba.
Siku ya walinzi wako imewadia,
siku atakayokutembelea Mungu.
Sasa ni wakati wao
wa kuchanganyikiwa.

5 Usimtumaini jirani;
usiweke matumaini kwa rafiki.
Hata kwa yule alalaye kifuani mwako
uwe mwangalifu kwa maneno yako.

6 eKwa kuwa mwana humdharau baba yake,
naye binti huinuka dhidi ya mama yake,
mkwe kuwa kinyume na mama mkwe wake:
adui wa mtu ni wale wa nyumbani mwake hasa.


7 fLakini mimi, namtazama Bwana kwa matumaini,
namngoja Mungu Mwokozi wangu;
Mungu wangu atanisikia mimi.

Israeli Atainuka


8 gUsifurahie msiba wangu, ee adui yangu!
Ingawa nimeanguka, nitainuka.
Japo ninaketi gizani,
Bwana atakuwa nuru yangu.

9 hKwa sababu nimetenda dhambi dhidi yake,
nitabeba ghadhabu ya Bwana,
mpaka atakaponitetea shauri langu
na kuithibitisha haki yangu.
Atanileta nje kwenye mwanga,
nami nitaiona haki yake.

10 iKisha adui yangu ataliona
naye atafunikwa na aibu,
yule aliyeniambia,
“Yu wapi Bwana Mwenyezi Mungu wako?”
Macho yangu yataona kuanguka kwake,
hata sasa atakanyagwa chini ya mguu
kama tope barabarani.


11 jSiku ya kujenga kuta zako itawadia,
siku ya kupanua mipaka yako.

12 kSiku hiyo watu watakuja kwako
kutoka Ashuru na miji ya Misri,
hata kutoka Misri hadi Frati
na kutoka bahari hadi bahari
na kutoka mlima hadi mlima.

13 lDunia itakuwa ukiwa kwa sababu ya wakazi wake,
kwa sababu ya matunda ya matendo yao.

Sala Na Sifa


14 mWachunge watu wako kwa fimbo yako,
kundi la urithi wako,
ambalo linaishi peke yake msituni,
katika nchi ya malisho yenye rutuba.
Waache walishe katika Bashani na Gileadi
kama ilivyokuwa siku za kale.


15 n“Kama siku zile mlipotoka Misri,
nitawaonyesha maajabu yangu.”


16 oMataifa yataona na kuaibika,
waliondolewa nguvu zao zote.
Wataweka mikono yao kwenye vinywa vyao
na masikio yao yatakuwa na uziwi.

17 pWataramba mavumbi kama nyoka,
kama viumbe vitambaavyo juu ya ardhi.
Watatoka nje ya mapango yao wakitetemeka;
watamgeukia Bwana Mwenyezi Mungu wetu kwa hofu
nao watakuogopa.

18 qNi nani Mungu kama wewe,
ambaye anaachilia dhambi
na kusamehe makosa
ya mabaki ya urithi wake?
Wewe huwi na hasira milele,
bali unafurahia kuonyesha rehema.

19 rUtatuhurumia tena,
utazikanyaga dhambi zetu
chini ya nyayo zako,
na kutupa maovu yetu yote
katika vilindi vya bahari.

20 sUtakuwa wa kweli kwa Yakobo,
nawe utamwonyesha Ibrahimu rehema,
kama ulivyowaahidi kwa kiapo baba zetu
siku za kale.
Copyright information for SwhKC